Jeshi la Polisi mkoa wa Arusha limewafukuza kazi askari wanne na kuwasimamisha kazi wakaguzi wawili wa polisi ambao wanatuhumiwa kuomba na kupokea rushwa ya shilingi milioni 100.

Taarifa hiyo imetolewa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha ACP Justine Masejo, na kueleza kuwa tukio hilo la kuomba rushwa walilitekeleza Machi 19, 2021, maeneo ya Arumeru.

Aidha Kamanda Masejo ameongeza kuwa wakaguzi pamoja na askari hao watakabidhiwa kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), mkoani humo kwa ajili ya kuendelea na taratibu za kiuchunguzi.

Inadaiwa kuwa askari hao waliomba rushwa kwa Profesa Justine Maeda, ambaye amewahi kuwa mshauri wa uchumi wa Rais wa awamu ya kwanza, Hayati Julius Nyerere, baada ya kumpekua nyumbani kwake na kukuta vipande viwili vya meno ya Tembo kwenye mzinga wa Nyuki.