Na Teresia Mhagama, Dar es Salaam
Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani ameagiza kuwa, matengenezo ya mitambo mbalimbali ya kufua umeme nchini yakamilike ndani ya siku Tano ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata umeme wa uhakika.

Dkt. Kalemani ametoa agizo hilo tarehe 2 Machi, 2021 mkoani Dar es Salaam,  mbele ya Bodi na Menejimenti za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Songas, baada ya kukagua kituo cha umeme cha Songas ambacho mitambo yake miwili inafanyiwa matengenezo na hivyo kuzalisha umeme wa kiasi cha megawati 115 badala ya 180.

Akiwa ameambatana na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Leonard Masanja, Waziri Kalemani amesema kuwa, hataki kusikia wananchi wakilalamika kukosa umeme kwa sababu tu ya matengenezo ya mitambo, hivyo matengenezo hayo yakamilike ndani ya siku alizoagiza au kwa siku chache zaidi.

Aidha, kuhusu muda wa kufanya matengenezo ya mitambo ya umeme nchini, Dkt. Kalemani ameiagiza TANESCO na Songas kupishanisha muda wa matengenezo ili kutoathiri hali ya upatikanaji wa umeme nchini.

Vilevile, Dkt.Kalemani alisisitiza kuhusu utekelezaji wa agizo alilolitoa kwa TPDC la kuhakikisha kuwa vifaa mbalimbali vinavyotumika kwenye miundombinu ya gesi nchini kama vile valvu na mabomba vinatengenezwa nchini ili kurahisisha upatikanaji wa vifaa husika.

Vilevile, amesema kuwa, Wizara ya Nishati haitaacha kufuatilia kwa karibu utendaji kazi wa Taasisi zilizo chini yake kwani lengo ni kuhakikisha kuwa Taasisi hizo zinafanya kazi kwa ufanisi na wananchi wanapata huduma wanazostahili.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa Songas, Anael Samuel, alimueleza Waziri wa Nishati kuwa, matengenezo ya mitambo miwili ya umeme kwenye kituo hicho, yanaenda sambamba na matengenezo katika bomba la Gesi kutoka Songosongo linalopeleka gesi kwenye mitambo hiyo ya Songas ili kuzalisha umeme.

Alisema kuwa, kutokana na bomba hilo la gesi kutoka Songosongo kufanyiwa matengenezo, kwa sasa megawati 115 zinzozalishwa kwenye kituo hicho zinatokana na mitambo ya gesi ya Shirika la Maendeleo Tanzania (TPDC).

“Nazipongeza Taasisi za TPDC na TANESCO kwa kushirikiana na Songas kwani tulikaa pamoja kama wadau ili kuona namna tutakavyotatua tatizo hili, na ndiyo maana angalau megawati 115 zinaendelea kuzalishwa kwa kutumia mitambo ya TPDC.” Alisema Samuel

Aidha, alisema kuwa, ukarabati wa mitambo hiyo unafanyika kwa ratiba maalum ili kuweza kutoa uhakika wa mitambo hiyo kuendelea kuzalisha umeme kwa muda mrefu zaidi.

Kwa upande wake, Meneja Mitambo wa Songas, Michael Mngodo alisema kuwa kituo cha umeme cha Songas kina mashine Sita ambapo kwa sasa mashine zinazofanya kazi ni nne na zinazofanyiwa matengenezo ni mashine mbili