Na. Edward Kondela
Balozi wa Falme za Nchi za Kiarabu (U.A.E) hapa nchini Mhe. Khalifa Almarzooqi Abdulrahman amesema ataandaa wajumbe kutoka U.A.E kuja hapa nchini kutembelea viwanda vya kuchakata nyama ili kujiridhisha na ubora wa nyama kwa ajili ya kupeleka katika nchi zao.

Akizungumza leo (03.03.2021) na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki, mara baada ya kumtembelea katika ofisi ndogo za wizara hiyo zilizopo jijini Dar es Salaam, balozi huyo amesema ni muhimu kwa viwanda vya kuchakata nyama vilivyopo hapa nchini kupata soko la uhakika katika nchi za Falme za Kiarabu kwa kuzingatia Tanzania ni nchi ya pili kwa kuwa na idadi kubwa ya mifugo.

Aidha, amewaasa wamiliki wa viwanda hivyo kuketi pamoja na kuwa na umoja wao katika kukabiliana na changamoto mbalimbali ikiwemo ya kutafuta masoko ya bidhaa zao.

Kwa upande wake Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amemweleza balozi huyo kuwa viwanda vingi vya kuchakata nyama vinakabiliwa na changamoto ya masoko kupeleka bidhaa zao nchi za nje kutokana na kudaiwa kukosa sifa kulingana na baadhi ya sheria na kanuni zilizopo katika nchi hizo za kuingiza nyama kutoka nchi za nje.  

“Viwanda vyetu vya kuchakata nyama licha ya kuwa na uwezo mkubwa wa kuchinja idadi kubwa ya ng’ombe, mbuzi na kondoo lakini bado vinakabiliwa na changamoto ya kukosa masoko ya kupeleka bidhaa zao mara baada ya kuchakata nyama.” Amesema Mhe. Ndaki

Kuhusu ujumbe kutoka Falme za Nchi za Kiarabu (U.A.E) kuja nchini kutembelea viwanda vya kuchakata nyama na kujiridhisha na ubora wa bidhaa zinazozalishwa kama alivyoahidi balozi wa U.A.E hapa nchini Mhe. Khalifa Almarzooqi Abdulrahman, Waziri Ndaki amesema ujumbe huo utakuwa ni mwanzo mzuri wa viwanda hivyo kupata masoko ya bidhaa zao nchi za nje.

Pia, Waziri Ndaki kuhusu sekta ya uvuvi amemwambia balozi huyo kuwa serikali iko katika hatua mbalimbali za kuhakikisha uvuvi wa bahari kuu unaanza katika ukanda wa Bahari ya Hindi kwa kujenga bandari ya uvuvi pamoja na ununuzi wa meli za uvuvi.