TUME ya Taifa ya Uchaguzi imetangaza Ratiba ya uchaguzi mdogo wa Ubunge wa Jimbo la Muhambwe, mkoani Kigoma baada ya kupokea Barua kutoka kwa Spika wa Bunge kuwa kiti hicho kiko wazi.

Taarifa iliyotolewa kwa Vyombo vya habari Jijini Dodoma leo, 27 Machi, 2021, na kusainiwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Dkt. Willson Mahera amesema uchaguzi huo umeapangwa kufanyika tarehe 2 Mei, 2021.

“Tume ilipokea barua kutoka kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambaye kwa kuzingatia kifungu cha 37 (3) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343, ameitaarifu Tume uwepo wa nafasi wazi ya kiti cha Ubunge katika Jimbo la Muhambwe, Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo, Mkoani Kigoma,” alisema Dkt Mahera.

Aidha, kwa kuzingatia kifungu cha 37 (1) (b), cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, sura ya 343 ambacho kinaitaka Tume kujaza nafasi ya kiti cha Ubunge katika kipindi kisichopungua siku 20 na kisichozidi siku 50 tangu kutokea kwa sababu iliyoacha nafasi wazi ya kiti hicho.

“Kutokana na matakwa hayo ya kisheria, Tume inautaarifu Umma kuwa Jimbo la Muhambwe liko wazi na uteuzi wa wagombea utafanyika tarehe 3 Aprili, 2021 Hivyo, uchaguzi ambayo ni siku ya 49 tangu kutokea kwa kifo hicho,”alisema Dkt. Mahera.

Alisema kuwa maandalizi kwaajili ya uchaguzi huo yameshafanyika na kazi ya utoaji fomu za uchaguzi kwa wagombea inaanza 28 Machi hadi 3 Aprili, 2021 huku uteuzi wa wagombea watakao wania nafasi hiyo ukifanyika 3 Aprili mwaka huu.

Aidha Dkt Mahera amesema kampeni za uchaguzi katika jimbo hilo zitaanza 3 Aprili 2021 na zitafikia ukomo wake Mei mosi mwaka huu na uchaguzi kufanyika 2 Mei, 2021.

Mahera alisema yayari Tume imekwisha vitaarifu Vyama vya Siasa kwa njia ya barua juu ya kuwepo kwa uchaguzi huo mdogo na inavikumbusha kuzingatia sharia, kanuni, Maadili ya Uchaguzi, Miongozo na Maelekezo ya Tume wakati wote wa kipindi cha Uchaguzi.

Pia Mahera alitumia fursa hiyo kutoa salamu za pole kwa viongozi wa Serikali, Familia na Watanzania wote kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt John Pombe Magufuli.

“Tume inatoa pole kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, Familia ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Chama cha Mapinduzi na watanzania wote kwa ujumla,” alisema Dkt Mahera.

Uchaguzi katika jimbo la Muhambwe unafanyika baada ya Mbunge wa Muhambwe (CCM) mkoani Kigoma Atashasta Justus Nditiye kufariki dunia Februari 12, 2021 ambaye alifariki akiwa Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma alikokuwa akipatiwa matibabu baada ya kupata ajali ya gari eneo la Name name jijini humo Februari 11, 2021.