Mkurugenzi Mkuu Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Brigedia Generali John Mbungo amesema wamefanikiwa kutekeleza mapambano dhidi ya rushwa kwa 89.8% kwa mwaka 2019/2020 tofauti na mwaka 2018/2019 ambapo walifikia 88.1%.

Mbungo amebainisha hayo wakati akikabidhi ripoti yake kwa Rais, Samia Suluhu Hassan katika Ikulu ya Chamwino Jijini Dodoma mapema hii leo.

Amesema mafanikio hayo yamekuja kutokana na kutoa elimu kwa umma kuhusiana na madhara ya rushwa kwa wananchi ambapo semina zipatazo 3683 zilitolewa na kusaidia majalada 1079 kukamilika tofauti na mwaka uliopita ambapo yalikuwa 911.

 “Kati ya majalada hayo majalada 385 yalihusu hongo na majalada mengine 694 yalihusu vifungu vingine vya sheria vya kuzuia na kupambana na rushwa” amesema Mbungo.

Aidha, amebainisha kuwa hadi majalada hayo uchunguzi wake   unakamilika uligusa sehemu mbalimbali ikiwemo ukiukwaji wa sheria ya manunuzi ya umma, vyama vya ushirika vya masoko ya mazao ya kilimo kutowalipa wakulima baada ya kuuza mazao yao kwenye vyama hivyo, mikopo umiza na ufujaji wa fedha katika miradi ya maendeleo.