Na Stella Kalinga, Simiyu RS
Serikali imeanza maandalizi ya ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) kipande cha Mwanza-Isaka yenye urefu wa kilomita 341 ambayo itajengwa kwa gharama ya shilingi trilioni 3.0267 fedha za ndani, ambapo katika mradi huu Bandari kavu na stesheni  vinatarajiwa kujengwa katika eneo la Malampaka wilayani Maswa mkoani Simiyu..

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Bw. Masanja Kadogosa Machi 08, 2021 katika kikao cha pamoja cha wadau ambacho kilifanyika katika Chuo cha Maendeleo ya Jamii Malampaka wilayani Maswa kwa lengo la kujenga uelewa wa pamoja juu ya utekelezaji wa mradi huu ili  kufanya maandalizi muhimu.

“Hapa Malampaka tutakuwa na kambi ya watu zaidi ya 3000 kwa hiyo ni vizuri wananchi wakaandaliwa ili waweze kushiriki fursa mbalimbali, tunatarajia pia kujenga bandari kavu kama ilivyo Isaka mizigo kutoka mikoa mbalimbali itaishia hapa; Malampaka pia tutajenga stesheni jengo kubwa lenye mita za mraba 8000 ambayo ndani itakuwa na benki, maduka na huduma nyingine,” alisema Kadogosa.

“Mradi huu ni lazima uwe na maana kwa maisha ya watu wa kawaida, mahitaji mbalimbali yatahitajika na watenda kazi kwenye mradi huu kama vile malazi, chakula mfano kuku tu zitahitaji zaidi ya kuku 40,000 kwa mwezi, kwa hiyo hii ni fursa nzuri itakayobadilisha maisha ya wengi, wananchi wajipange kutumia fursa hii,” alisisitiza.

Aidha, Kadogosa ametoa wito kwa wananchi na wadau wengine kutoka taasisi mbalimbali kushirikiana na TRC ili utekelezaji wa mradi huu usiathiri shughuli mbalimbali za wananchi na taasisi hizo zinazotoa huduma kwa jamii, huku akiahidi kuwa TRC itaendelea kusimamia upatikanaji wa fursa zipatikane kwa usawa kama ilivyoelekezwa na Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema mkoa wa Simiyu umepokea mradi huo kwa asilimia 100 na kuahidi kutoa ushirikiano, huku akiwahakikishia usalama wakandarasi na watu wote watakaohusika na utekelezaji wa mradi huu.

Kiswaga ameagiza idara ya ardhi Maswa kupima maeneo ili wananchi waweze kupata maeneo ya kujenga na kuwekeza kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali, ambapo pia ametoa wito kwa wananchi kununua maeneo hayo yatakapotangazwa, ili waweze kujenga nyumba za kuishi na kuwekeza katika fursa mbalimbali kuinua uchumi wao, mkoa na Taifa kwa ujumla.

Katibu wa CCM mkoa wa Simiyu, Bi. Haula Kachwamba ametoa wito kwa Wananchi wa Malampaka kila mmoja kuwa mlinzi wa mali za mkandarasi na serikali, “ Hatutegemei mali ya serikali na mkandarasi ikaibiwa, tunategemea itafanya kazi iliyokusudiwa hivyo kila mmoja akawe mlinzi, lakini pia mjiandae kutumia fursa hii, wakulima, wafugaji, mama ntilie kila mmoja kwa namna yake.”

Mwenyekiti Kijiji cha Ikungu Bw. Chuma Gashi amesema wananchi wa Kijiji hicho wameupokea mradi huo kwa mikono miwili na wako tayari kupisha maeneo yatakayohitajika kwa kufuata taratibu huku akibainisha kuwa yeye binafsi kama mwananchi amejipanga kufanya biashara ya kuku katika kambi itakayojengwa Malampaka na baadaye reli ikikamilika atasafirisha kwenda Dar es salaam.

Naye Julia Musa amesema “mradi wa reli tumeupokea kwa furaha maana tunajua mji wetu wa Malampaka utapata maendeleo, vijana watapata ajira, tunamuombea Mhe. Rais azidi kutuletea miradi mingine ili sisi wana Malampaka tuzidi kupata maendeleo, tuko tayari kupisha mradi na kwenda kwenye maeneo tutakayopangiwa na serikali tukilipwa fidia ili kupisha ujenzi wa reli hii.”

Kwa mujibu wa Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Mhe. Aswege Kaminyoge amesema eneo la Malampaka linakadiriwa kuwa na wakazi wapatao 14,300.