Na.Catherine Sungura.WAMJW,Dodoma
Serikali imeendelea kuhakikisha upatikanaji wa dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi katika vituo vya kutolea huduma za afya unakuwa wa kuridhisha.


Hayo yameelezwa jana  na Waziri wa Afya Dkt. Dorothy Gwajima wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya wizara (Idara Kuu ya Afya) kwa kipindi Cha Julai 2020 Hadi Februari,2021 Kwenye  kamati ya kudumu ya Bunge ya huduma na maendeleo ya Jamii jijini Dodoma.


Dkt.Gwajima amesema katika kuhakikisha kuwa dawa zinapatikana kwa wakati na zenye ubora,Serikali ilitenga kiasi Cha shilingi Bilioni 200 katika kipindi Cha mwaka 2020/2021 kwa ajili ya ununuzi wa dawa,vifaa,vifaa tiba na vitendanishi.


Aidha,Dkt. Gwajima amesema upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya  kwa aina 312 za Dawa upatikanaji umefikia kiasi Cha asilimia 74.


Hata hivyo amesema Wizara ya Afya imeboresha huduma za afya ya uzazi nchini  katika kipindi Cha Julai 2020 Hadi Februari 2021  ambapo jumla ya wajawazito 1,165,526(sawa na asilimia 103 ya waliotarajiwa) walihudhuria kliniki na kupata huduma.


“Kati ya wajawazito hao asilimia 36.5 ndio walianza huduma kabla ya wiki 12 ikilinganishwa na asilimia 36.4 kipindi Kama hiki mwaka 2019”.


Aliongeza kuwa asilimia 90.4 walifanya mahudhurio manne au zaidi ikilinganishwa na asilimia 84.1 mwaka 2019.


Kwa upande wa waliojifungulia katika vituo vya kutolea huduma za afya Dkt. Gwajima amesema wajawazito 920,126 sawa na asilimia 82 Kama ilivyokua katika kipindi Kama hicho mwaka 2019.


Aliongeza kuwa katika kuimarisha huduma za Kinga hususan huduma za Chanjo jumla ya Watoto wa chini ya mwaka mmoja 1,030,617 walitegemewa kupatiwa chanjo kwa ajili ya kuwakinga na Magonjwa mbalimbali na Hadi kufukia Februari 2021 Watoto 1,010,005 sawa na asilimia 98 walipatiwa chanjo kwa kutumia kigezo Cha PENTA-3 kwa mujibu wa mwongozo wa Shirika la Afya Duniani(WHO).