Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam, -Aboubakar Kunenge amewashukuru Wakazi wa mkoa huo kwa kujitokeza kwa wingi kutoa heshima zao za mwisho kwa aliyekuwa Rais wa Tanzania Dkt John Magufuli.


Kunenge amesema kuwa, wingi wa watu waliojitokeza kutoa heshima zao za mwisho jana  unathibitisha kuwa Marehemu Rais Magufuli alikuwa ni kipenzi cha watu wa Dar es salaam na kwamba hiyo ni heshima ya juu kwa kiongozi huyo.

Akizungumza na Waandishi wa habari jana katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere mara baada ya kukamilika kwa shughuli ya kuusafirisha mwili wa Dkt Magufuli kwenda mkoani Dodoma, Kunenge alisema Wakazi wa Dar es salaam wamemtendea haki Marehemu Dkt Magufuli kwa namna walivyojitokeza.

Kunenge aliongeza kuwa Wakazi wa Dar es salaam wameguswa na maisha ya Dkt Magufuli, ndio maana wamejitokeza kwa wingi kumpa heshima yake katika siku zote mbili walizopewa nafasi ya kumuaga katika uwanja wa Uhuru.