Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan amewaongoza viongozi waandamizi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar akiwemo Rais Dkt Hussein Ali Mwinyi kusaini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli huku baadhi ya mabalozi wakibubujikwa na machozi.

Rais Samia Suluhu Hassan amesaini kitabu cha maombolezo katika viwanja vya Kamrijee Dar es Salaam mchana wa leo na kufuatiiwa na baadhi ya mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao hapa Tanzania kufuatia kifo cha aliyekuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Joseph Magufuli aliyefariki dunia Machi 17, 2021 katika hospitali ya Mzena kwa maradhi ya moyo.

Pia Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe Hussein Ally Mwinyi nae pia amesaini kitabu cha maombolezo akifuatiwa na Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe Othaman Masoud

Baadhi ya Mabalozi wanaoziwakilisha Nchi zao hapa Nchini walishindwa kujizuia na kutokwa na machozi kumlilia Hayati Dkt. Magufuli na kumuelezea kuwa alikuwa kiongozi jasiri na mzalendo si kwa manufaa ya Tanzania pekee bali Afrika kwa ujumla ambapo Balozi wa Jamaica hapa nchini Mhe. Velisa Delfosse amemuelezea Hayati Dkt Magufuli kama mwanampinduzi na mzalendo halisi wa Afrika wa wakati huu

“Rais Magufuli alikuwa mwanampinduzi na mzalendo halisi wa Afrika wa wakati huu, kwa kweli tumeguswa sana na msiba wake hakika pengo lake halitazibika, tunamuombea kwa Mungu apumzike salama,” Amesema Balozi Delfosse

Nae Balozi wa China hapa Nchini Mhe. Wang Ke mara baada ya kusaini kitabu cha maombolezo amemuelezea Hayati Magufuli kama kiongozi mwenye maono na mzalendo mwaminifu kwa Afrika,na kwamba atakumbukwa na Watanzania kwa jitihada zake kubwa za kuleta mabadiliko chanya  ili kuinua hali ya maisha hususani wale wa kipato cha chini.

Kwa upande wake Balozi wa Sudani ya Kusini Mhe. William Ruben amewasihi viongozi wa Afrika na Watanzania kwa ujumla kufuata nyayo za Hayati Dkt Magufuli kwa kuwa alikuwa alama halisi ya Afrika na alitufundisha wengi wetu kuamini kuwa Afrika imebarikiwa na ni tajiri kinyume na tulivyoamini kuwa tunahitaji msaada kutoka kwa mataifa ya nje ya bara la Afrika

“Naomba kuwasihi viongozi wa Afrika na Watanzania kwa ujumla kufuata nyayo za Hayati Dkt Magufuli kwa kuwa alikuwa alama halisi ya Afrika na alitufundisha wengi wetu kuamini kuwa Afrika imebarikiwa na ni tajiri kinyume na tulivyoamini kuwa tunahitaji msaada kutoka kwa mataifa ya nje ya bara la Afrika,” Amesema Balozi Ruben

Mabalozi wengine waliofika katika viwanja vya Karimjee na kusaini kitabu cha maombolezo ni pamoja na Balozi wa Morocco Mhe Abdililah Benryane, Balozi wa Ethiopia Mhe Yonas Sanbe, Balozi wa Qatar Mhe Abdulla Jassim Al Madadadi, Balozi wa Japan Mhe Shinichi Goto Balozi wa Palestina Mhe Derar Ghannan, Balozi wa Cuba Mhe Lucas Damingo, Balozi wa Pakistan Mhe Mohammed Salem, Balozi wa Uswis Mhe Didier Chassot, Balozi wa Ireland Mhe Mary Oneill.

Wengine ni Balozi wa Rwanda Meja Jeneral Charles Karamba, Balozi wa Syria Dr Sawsan Alani, Balozi wa Korea Mhe Kim Yong Su, Balozi wa Iran Mhe Hussein Alvandi Behined, Balozi Uhispania Mhe Fransisca Pedros na Balozi Vietnam Mhe Nguyen Namtien.

Baadhi ya Wakuu wa mashirika na Taasisi za Kimataifa waliofika kusaini kitabu cha maombolezo ni pamoja na Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa Mhe. Zlatan Milisic, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto duniani UNICEF, Mhe. Shahini Bahuguna, Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni Mhe Tirso Do Santos, Shirika la Kazi duniani Wellingtone Chibebe, Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa Mhe Christine Musisi na Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa Mhe Antonio Jose Canandula.