Rais wa Tanzania Samia Suluhu amesema mazishi ya Dk John Magufuli  yatafanyika Machi 25, 2021 Wilaya ya Chato mkoani Geita.

Ametangaza siku  ya  mazishi muda mfupi baada kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania akichukua nafasi ya Magufuli aliyefariki dunia  Machi 17,  2021.

Akielezea ratiba nzima ya mazishi amesema Machi 20 mwili utatolewa hospitali ya Lugalo na kupelekwa Kanisa la St Peters kwa ibada na kisha  kupelekwa uwanja wa Uhuru kwa ajili ya kuagwa na viongozi.

Machi 21 mwili utaagwa na wakazi wa  Dar es Salaam katika uwanja huo huo na baadaye  utasafirishwa kuelekea Dodoma.

Machi 22 mwili utaagwa Dodoma kuanzia saa tatu asubuhi na siku hiyo itakuwa  ya mapumziko.

Machi 23, 2021 mwili utaagwa Mwanza na kisha kusafirishwa kuelekea Chato ambako utaagwa siku ya Jumanne ya Machi 24, 2021.

“Machi 25 mazishi yatafanyika baada ya misa takatifu itakayofanyika katika kanisa katoliki Chato na siku hii itakuwa ya mapumziko,” amesema Samia.