Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya ametoa salamu za pole kwa Serikali ya Tanzania na Watanzania wote kufutia kifo cha Rais Dkt John Magufuli kilichotokea hapo jana mkoani Dar es salaam.

Akilihutubia Taifa la Kenya kufuatia msiba wa Rais Magufuli, Rais Kenyatta amesema Kenya  imesikitishwa na kifo cha Rais Maguful.

Amesema binafsi alikuwa akishirikiana kwa karibu na Rais Magufuli na kuongeza kuwa amepoteza ndugu, rafiki na Kiongozi mwenzake.

“Ninakumbuka mara nyingi tulikutana na kuongea kuhusu maendeleo ya nchi zetu mbili, safari yake rasmi alipotembelea Kenya tulifungua barabara na pia alinipatia heshima kubwa sana kwa kumtembelea mama yangu na pia alinialika Tanzania ambapo na mimi pia nilipata fursa ya kutembelea Chato na kuonana na mama yake na tulilala pale nyumbani kwake na kufanya mazungumzo ya kina kuhusu uhusiano wetu kama wanachama wa Afrika Mashariki."-Kenyatta

Amesema Kenya iko pamoja na Tanzania katika kuomboleza msiba huo mkubwa na itaendelea kushirikiana na Tanzania hadi siku ya kupumzishwa kwa Dkt Magufuli katika nyumba yake ya milele.

“Asubuhi ya leo nilipata nafasi ya kungea na Makamu wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan na kumpa pole na kumhakikishia kwamba tutaendelea kushirikiana na serikali ya Tanzania hadi kuhakikisha kwamba tumempuzisha rafiki yetu na kuendela na msimamo wake wa kuunganisha wananchi wa Afrika Mashariki,” amesema Rais Kenyatta.