Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya amemweleza Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kuwa, aliyekuwa Rais wa Tanzania Dkt John Magufuli amefungua barabara ya maendeleo Tanzania ambayo anapaswa kuifuata.


Rais Kenyatta amemtia moyo Rais Samia na kusema kuwa, licha ya kupokea uongozi katika kipindi kigumu cha majonzi,  Mwenyezi Mungu ataendelea kuwa pamoja naye na kumsaidia, hivyo anapaswa kuwa na moyo mkuu.

Amewataka Watanzania kuendeleza falsafa ya Dkt Magufuli ya Hapa Kazi Tu, ambayo imesaidia kuleta mabadiliko katika nchi ya Tanzania na kuhamasisha maendeleo katika eneo lote la Afrika Mashariki.

Kenyatta ambaye kwa sasa ndiye Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) amesema kuwa, nchi zote za Ukanda wa Afrika Mashariki zipo pamoja na Tanzania kuomboleza msiba huo mkubwa wa Dkt Magufuli.