Baraza Maalum la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa, hivi karibuni limepitisha Bajeti ya  yenye thamani ya shilingi bilioni 22,709,154,050.00,  kwa mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya Halmashauri, katika  kikao kilichofanyika , Ukumbi wa Kepten John Komba Uliopo Mbamba bay Wilayani hapa.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa Bw. Stewart Nombo,  ambaye  pia ni mwenyekiti wa baraza la Madiwani  amesema kuwa baraza  limeidhinisha  mpango na bajeti ya maendeleo, kwa mwaka wa fedha 20212022,  kwa kuwa bajeti hii imelenga kutatua kero mbalimbali za wananchi, ikiwa ni pamoja na kutekeleza Miradi ya Maendeleo, na kutoa wito kwa   madiwani  kutoa ushirikiano kwa wataalamu  katika usimamizi wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Kata zao.

Akiwasilisha Mapendekezo ya Mpango wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2021 2022,  Kwa niaba ya Mkurugenzi mtendaji Wilaya ya Nyasa, Ofisa Mipango wilayani wa Wilaya Bw. Jabir Chilumba amefafanua kuwa bajeti hiyo, inalenga kutekeleza Program mbalimbali zilizopangwa kufanyika katika Halmashauri. Kati ya Kiasi hiki Tsh 1,237,512,500.00 sawa na Asilimia 5.45, ni makusanyo ya ndani, Tsh 13,283,311,000.00 sawa na Asilimia 58.49 ni kwa ajili ya Mishahara, Tsh 1,425,032,000.00 sawa na asilimia 6.28 kwa ajili ya matumizi mengineyo, na  Tsh 6,763,298,550.00 sawa na asilimia 29.78 kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa Bw Jimson Mhagama,  amewataka madiwani wa Wilaya ya Nyasa kusimamia miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao, kwa kushirikiana na wananchi, kutekeleza miradi hiyo na kusema kuwa Miradi hii inatekelezwa kwa fedha za walipa kodi, kwa hiyo ni jukumu la kila kiongozi kusimamia fedha hizo ili kujiletea maendeleo.

“waheshimiwa  madiwani ninawataarifu kuwa kila ninapokuandikia na kukupa taarifa za kukuletea fedha katika eneo lako, ni jukumu lako kusimamia, kuwashirikisha wananchi, na kutekeleza miradi kwa ubora wa hali ya juu, kwa kuwa fedha zinazotekeleza miradi hii ni kodi za wananchi wetu na Mh Rais amezileta ili zitatue changamoto za wananchi hivyo kila kiongozi anatakiwa kuwajibika kwa nafasi yake” .

Mhagama amesisitiza kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa, inatekeleza mpango mkakati wa kuongeza mazao ya kilimo na Biashara kwa kuongeza uzalishaji wa zao la kahawa, michikichi, Cocoa, Korosho na mazao mengine ili wananchi wanufaike na mazao ya kimkakati na Halmashauri iweze kupata mapato yanayotokana na mazao hayo.

Naye Mbunge wa Jimbo la Nyasa Mhandisi Stella Manyanya,  amesema Wilaya ya Nyasa ina mazao bora yasiyotumia mbolea za kiwandani, hivyo mazao hayo kwa sasa yamepata umaarufu mkubwa hasa  kwa   zao la kahawa, wanywaji wengi wa kahawa hawahitaji kahawa iliyolimwa kwa mbolea za kiwandani, wanahitaji mazao yaliyolimwa kwa kutumia samadi hivyo kwa Wilaya ya Nyasa tunatakiwa kutumia Fursa hiyo kwa kuvutia wawekezaji ili tuweze kujipatia maendeleo.

Aidha  amepongeza Mkurugenzi wa Mtendaji wa Wilaya ya Nyasa Bw Jimson Mhagama,  na Wataalamu wake, walioshiriki kuandaa mpango na bajeti  ambayo imezingatia vigezo  muhimu vyenye lengo la kutatua Kero za wananchi Wilayani Hapa.

Imeandaliwa na.

Netho Sichali

Afisa Habari  Wilaya ya Nyasa.