Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema  Wananchi wa Mkoa wa Dar es salaam na mikoa jirani leo  Machi 20 na kesho Machi 21, 2021 watapata fursa ya  kushiriki Ibada  ya kumwombea Hayati Dkt. John Pombe Magufuli na kutoa heshima za mwisho katika uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya kukagua maandalizi ya tukio jana Ijumaa, Machi 19, 2021, Mheshimiwa Majaliwa  amesema ameridhishwa na maandalizi  yanayofanywa chini ya usimamizi wa Kamati  ya Kitaifa ya Maafa ambayo yeye mwenyewe ndiye Mwenyekiti wake  akishirikiana  na Makamu wa Pili wa Rais wa  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla.

Mheshimiwa Majaliwa amesema Ibada hiyo itatanguliwa  na ibada nyingine  itakayofanyika kwenye Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro, Oysterbay jijini Dar es salaam ambako marehemu amekuwa akiabudu wakati wote alioishi Dar es salaam.

Amesema wananchi wote wa Mkoa wa Dar es Salam na mikoa jirani wanaotamani  kumuaga aliyekuwa rais wao mpendwa ambaye amefanya mambo mengi na makubwa  jijini Dar es salaam na Tanzania  kwa ujumla wafike uwanja wa Uhuru kuanzi saa 11 alfajiri amabapo watapokelewa na kuonyeshwa mahali pa kukaa.

Mheshimiwa Majaliwa amesema fursa ya kutoa heshima za mwisho itatolewa hadi saa 12 jioni na endapo itaonekana kuwa bado wapo watu wengi wanaotamani kutoa heshima za mwisho kwa mpendwa wao muda utaongezwa hadi  watakapomalizika.

Amesema Machi  22, 2021  mwili wa marehemu utasafirishwa kwenda Dodoma  ambako maombolezo ya kitaifa yatafanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri na waombolezaji wa mkoa wa Dodoma na mikoa ya jirani  pamoja na wambolezaji kutoka nje ya nchi watapata fursa  ya kushiriki  na kutoa heashima za mwisho.

Machi 23, 2021 asubuhi mwili  utasafirishwa  kwa ndege kutoka Dodoma kwenda Mwanza ambako  shughuli za maombolezo zitafanyika kwenye uwanja wa CCM Kirumba na wananchi  wa Mkoa wa Mwanza na mikoa jirani watapata fursa ya kutoa heshima za mwisho kwa marehemu.

Mheshimiwa Majaliwa amesema, Machi 24 mwili wa marehemu utasafirishwa kwenda Chato ambako wananchi wa Mkoa wa Geita na mikoa jirani watapata fursa ya kumuaga marehemu. Amesema  Machi 25 mapema asubuhi  itafanyika Ibada nyumbani kwa marehemu  Chato ikifuatiwa na mazishi.

Awali, Mheshimiwa Majaliwa alikwenda Ikulu  Ndogo jijini Dar es salam kutoa pole kwa Mjane wa Marehemu Mama Janet Magufuli  pamoja na  familia na baadae alikwenda kwenye Viwanja vya Karimjee kutia saini kitabu cha maombolezo.

Naye Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla amesema kuwa anafarijika kuona kwamba siku zote umekuwepo ushirikiano wa dhati kati Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika nyakati za shinda na raha.