Aliyekuwa Waziri wa Fedha Dkt. Philip Mpango ambaye ameteuliwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amemshukuru Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan na kusema amepigwa na butwaa na hakuwahi kuota.

''Namshukuru Rais Mhe. Samia Suluhu kwa kupendekeza jina langu na kuridhiwa na chama chetu cha CCM kuwa Makamu wa Rais, sikuwahi kuota, nimepigwa na butwaa,'' amesema Dkt. Philip Mpango.
 

Waziri huyo wa Fedha na Mipango ameeleza hayo leo Jumanne Machi 30, 2021 mara baada ya Spika wa Bunge, Job Ndugai kutangaza jina lake katika kikao cha kwanza cha Bunge la 12.

Huku akizungumza kwa umakini, amesema; “Hii ni nafasi muhimu sana na nyeti ya makamu wa rais ni heshima kubwa sana sikuwahi kuota, wakati naibu wangu anajibu swali nilikuwa nahangaika kwenye mambo mengine ikiwemo mishahara ya baadhi ya wabunge, nimetoka nje mara kadhaa kujaribu kuhangaika lakini nimepigwa na butwaa.”

Baada ya mjadala wa wabunge kuhusu uteuzi huo, wabunge watapiga kura kuthibitisha jina la Dk Mpango.

Uteuzi huyo umekuja kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati. Dk. John Pombe Magufuli na aliyekuwa Makamu wake Mhe. Samia Suluhu Hassan kuapishwa kushika nafasi ya Rais kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo kufanya nafasi ya Makamu wa Rais iwe wazi na leo imejazwa rasmi.