Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro amewaonya na kuwataka vijana wanaoendesha pikipiki maarufu kama bodaboda, kufuata sheria na alama za barabarani ili kuepusha ajali zinazoweza kuepukika.

IGP Sirro amesema hayo leo akiwa Kiwangwa mkoani Pwani na kuzungumza na baadhi ya wananchi wa eneo hilo wakati akiwa njiani kuelekea mkoani Tanga, ambapo amesema kuwa, karibu asilimia 90 ya vifo nchini vinatokana na ajali za pikipiki.

Hata hivyo, IGP Sirro amewataka wananchi hususan vijana kuacha kujihusisha na uhalifu wa kutumia silaha, wizi wa mifugo na mazao na kuwataka kujihusisha na biashara halali hasa za ujasiriamali.

Akiwa mkoani Tanga, IGP Sirro amefanya ukaguzi wa eneo la uwanja wa mbinu za medani lililopo Mkomazi mkoani humo na kusema kuwa, jitihada kubwa zinaendelea kufanyika ikiwemo kujenga majengo ya kisasa  kwa ajili ya kufanya mafunzo ya utayari kwa askari wa Jeshi hilo.