Spika wa Bunge la Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Job Ndugai, amemkaribisha bungeni Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, huku akimhakikishia ushiriakiano na wabunge kwa ajili ya kuleta maendeleo ndani ya nchi.

Spika Ndugai ameyasema hayo jana  alipokuwa anatoa salamu za pole kwa niaba ya wabunge wote wa bunge la Tanzania pamoja na la wawikilishi la Zanzibar katika ibada ya mazishi ya kumuaga aliyekuwa Rais Hayati Dk. John Magufuli inayofanyika Chato Mkoani Geita.

"Kipekee sisi bunge tumuhakikishie Mhe. Rais wetu Samia Suluhu Hassan ushirikiano wa kila aina, tutasimama nae kwa kila ambalo tunaweza kufanya, kuhakikisha kwamba anafanikiwa na nchi yetu inafanikiwa zaidi na zaidi," alisema Ndugai.

Hayati Dk. John Magufuli alifariki dunia Machi 17, 2021 katika hospitali ya Mzena jijini Dar es Salaam kwa ugonjwa wa moyo na amezikwa jana  katika kijiji cha Mlimani kilicho katika wilaya ya Chato mkoani Geita.