WAKULIMA mkoani Ruvuma wamefanikiwa kuingiza zaidi ya shilingi bilioni 25 baada ya kuuza kilo 12,234,757 ya zao hilo kupitia mfumo wa stakabadhi ya mazao ghalani kuanzia msimu wa mwaka 2018/2019 hadi 2019/2020.

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme amesema katika kipindi hicho wakulima pia walifanikiwa kuuza kilo 1,499,077 zilizowaingizia zaidi ya shilingi bilioni moja na zao la mbaazi ambalo liliwaingizia zaidi ya shilingi bilioni 2.585 baada ya kuuza kilo 4,260,777.

“Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa mikoa ambayo imekuwa inatekeleza mfumo wa stakabadhi ya mazao ghalani,pia tuna mazao mawili ya kimkakati ambayo ni korosho na kahawa,yamekuwa yakiuzwa kupitia mfumo huu’’,alisema Mndeme.

Amesema mfumo huo umewanufaisha wakulima kwa kupata soko la uhakika na bei nzuri ya mazao yao na kwamba shughuli za kilimo katika msimu wa mwaka 2020/2021 zinaendelea vizuri ambapo wakulima wamelima mazao mbalimbali.

Kuhusu mbolea,Mkuu wa Mkoa amesema Mkoa kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mbolea Tanzania(TFRA) unaendelea kusimamia upatikanaji wa mbolea ili wananchi waweze kuzalisha chakula cha kutosha.

Hata hivyo amesema hadi kufikia Novemba 2020 jumla ya tani 31,624 za mbolea zilikuwa zimeingia mkoani Ruvuma kati ya mahitaji ya mbolea tani 50,524.50.

Mkoa wa Ruvuma umekuwa gwiji katika uzalishaji wa mazao ya chakula nchini,baada ya kushika nafasi ya kwanza kitaifa miaka miwili mfululizo,msimu wa mwaka 2018/2019 na 2019/2020.