Serikali imesema itahakisha miradi ya maji inakamilika kwa wakati kwa kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha ili jamii iweze kunufaika na huduma ya maji safi na salama kupitia mradi wa maji wa Mabokweni, katika Jiji la Tanga.

Kauli hiyo imetolewa jana  na Waziri wa Maji Mhe. Juma Aweso mara baada ya kutembelea mradi wa Maji wa Mabokweni unaotekelezwa katika Jiji la Tanga kufuatia ombi la Mbunge wa Tanga Mjini Mhe. Ummy Mwalimu ambae pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira).

Mhe. Ummy Mwalimu amesema mradi wa maji wa Mabokweni umekwama kwa muda mrefu na kusababisha wakazi wa maeneo hayo na vitongoji vya Mzizima na Chongoleani kukosa maji safi na salama.

“Mhe. Waziri wa Maji, hapa Tanga mjini maji yanapatikana isipokuwa katika maeneo machache, kukamilika kwa mradi huu kutawezesha kutatua kero ya maji ya muda mrefu kwa wananchi wangu” Ummy Mwalimu alisisitiza.

Amesema pia changamoto nyingine  inayowakabili wakazi wa Tanga mjini ni bili kubwa za maji ambapo baadhi yao wamesitishiwa hudumu hiyo kutokana na kutozwa bili kubwa zisizolipika.

Kwa upande wake Waziri wa Maji Mhe. Juma Aweso amesema azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha kuwa inaboresha upatikana wa huduma maji mijini na vijijini.

“Serikali ina wajibu wa kuhakikisha huduma ya maji inapatikana kwa wananchi wake haiwezekani bili za maji kuwa kubwa kiasi hiki, naagiza badala ya kuuziwa ndoo moja kwa shilingi mia moja, sasa iuzwe kwa Shilingi hamsini tu hapa Kibafuta” Aweso alisisitiza.

Amemuagiza Meneja wa RUWASA kuhakikisha fedha zitakazotolewa zinatumika kwa kazi iliyokusudiwa ili mradi huo ukamilike ndani ya muda mfupi.

Katika ziara ya siku moja ya kukagua miradi ya maji katika Jiji la Tanga, Waziri wa Maji Jumaa Aweso na Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini Mhe. Ummy Mwalimu wametembelea Mradi wa Maji wa Mabokweni katika Kijiji cha Kiruku.