Na Eleuteri Mangi, WHUSM- Arusha
Viongozi wa halmashauri wametakiwa kuhamasisha wananchi kuendelea kufanya mazoezi katika maeneo yao na asitokee mtu yeyote atakayebeza kazi ya kuhamasisha kufanya mazoezi kwa afya kuanzia ngazi za vijiji, halmashauri, mikoa hatimaye nchi nzima.

Hayo yamesemwa na Naibu Waiziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Abdallah Ulega leo Februari 27, 2021 wakati aliposhiriki mashindano ya Bonanza la michezo lililoandaliwa na Wilaya ya Arusha.

“Arusha mpo kwenye mstari sahihi, mnafanya jambo sahihi kabisa, endeleeni na utamaduni huu na msirudi nyuma, mmeonesha mfano na wengine wataendelea kuiga mpaka pale ambapo nchi nzima watu watakuwa wanafanya mazoezi” Naibu Waiziri Ulega.

Ameongeza kuwa mazoezi ni kwa ajili ya afya na utimamu wa mwili ili kujikinga na magonjwa yanayoambukiza, milipuko na magonjwa yasiyoambukliza amabayo ni maelekezo ya Viongozi wa kitaifa wakiongozwa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, Mkamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020 ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho kinaongoza dola ambayo inaelekeza Serikali za mitaa viongozi wasimamie wananchi wafanye mazoezi katika maeneo yao.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha Idd Kimanta amewasisitiza wanannchi wa mko huo kuendelea kufanya mazoezi katika vilabu vyao vya jogging katika maeneo yao ili kuongeza upendo miongoni mwa na kuimarisha afya zao na kuendelea na shughuli zao za kiuchumi kujiongezea kipato na kuinua uchumi wa taifa.

Bonanza hili linaloratibiwa kupitia ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Arusha ambalo hadi sasa limefanyika kwa mwezi mzima wa Februari 2021 likiongozwa na kaulimbiu “Uzalendo wetu ni kuitumikioa nchi yetu Tanzania” ambalo limehusisha michezo mbalimbali ikiwemo riadha, mipra wa miguu, mpira wa wavu, mpira wa pete, mchezo wa kukimbiza kuku, kumbia kwa magunia na michezo mingine ya jadi.