Serikali ya Marekani imetangaza kumuunga mkono Mwanauchumi wa Nigeria Ngozi Okonjo-Iweala kuongoza Shirika la Bishara Duniani (WTO), hatua inayofungua njia kwa Shirika hilo kupata Kiongozi wa kwanza Mwanamke na wa kwanza kutoka Afrika.

Uamuzi huo wa Marekani ni ishara nyingine ya utawala wa Joe Biden kujitenga na sera za Mtangulizi wake Donald Trump ambaye aliidhoofisha nafasi ya WTO Duniani pamoja na kupinga Iweala kuongoza Shirika hilo licha ya kuungwa mkono na Mataifa mengine wanachama.

Mjumbe wa masuala ya biashara wa Marekani amesema uamuzi wa kumuunga mkono Iweala umefikiwa kwa kuzingatia tajriba ya Waziri huyo wa zamani wa fedha wa Nigeria hasa katika masuala ya uchumi na diplomasia ya kimataifa.

Oktoba 2020 Mabalozi wa Mataifa makubwa ndani ya WTO walimuunga mkono Iweala kuongoza Shirika hilo lakini bila uungaji mkono wa Marekani mchakato wa uchaguzi ulisimama kwa sababu Mkurugenzi wa WTO huchaguliwa kwa maafikiano ya nchi zote 164 Wanachama.