Mwanasiasa Mkongwe nchini na waziri wa zamani wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Muhammed Seif Khatib (70), amefariki dunia hii leo Februari 15, 2021 mjini Unguja.

Taarifa za kifo cha Khatibu zimethibitishwa na Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo Zanzibar, Dk Juma Mohammed.

“Ni kweli amefariki leo asubuhi kwa mujibu wa taarifa za mwanawe, mwili wake uko kwenye hospitali ya Al-Rahma,” amesema Dk Mohammed

Taarifa zaidi zimesema Dk Khatib anatarajiwa kuzikwa kesho saa nne asubuhi huko Mpendae, Unguja.

Wakati wa uhai wake Khatib amewahi kuwa mbunge wa jimbo la Uzini, Unguja na amewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya CCM na nafasi kadhaa ndani ya serikali kama Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano na Mazingira na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Atakumbukwa kwa utaalamu wake wa lugha ya Kiswahili ambapo hadi anafariki dunia alikuwa ni Mwenyekiti wa Baraza la Kiswahili Zanzibar (Bakiza).