Mkazi wa Tabata, Lina Muro (46) amehukumiwa kwenda jela miaka 30 baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya zenye uzito wa gramu 43.95.

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mwandamizi , Agustina Mbando baada kupitia ushahidi wa upande wa mashtaka uliokuwa na mashahidi saba na kujiridhisha pasipo kuacha shaka yoyote.

Ilidaiwa kuwa Januari 26, 2018 katika maeneo ya Tabata Bima NSSF, mshitakiwa huyo alikutwa akisafirisha dawa za kulevya aina ya heroin zenye uzito wa gramu 43.95. 

Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Mbando alisema baada ya kupitia ushahidi wa mashahidi wote saba pamoja na vielelezo, Mahakama hiyo imejiridhisha pasipo shaka hivyo inamtia hatiani.

Hakimu Mbando alisema kutokana na ushahidi wa upande wa mashitaka uliotolewa, Mahakama inamtia hatiani hivyo atatumikia kifungo cha miaka 30 jela na kutaifisha simu nne alizokutwa nazo.