Rais wa Marekani Joe Biden ametangaza kuidhinisha amri ya kiutendaji ya kuwawekea vikwazo vipya wahusika wa mapinduzi ya kijeshi ya Myanmar na kusisistiza kurejeshwa demokrasia na kuwaachia viongozi wa kiraia.

Rais wa Marekani Joe Biden ametangaza kuidhinisha amri ya kiutendaji ya kuwawekea vikwazo vipya waliohusika na mapinduzi ya kijeshi nchini Myanmar na kurejelea wito wake wa kurejeshwa demokrasia pamoja na kuwaachia viongozi wa kiraia.

Biden amesema amri hiyo itawezesha utawala wake "kuwawekea vikwazo haraka viongozi wa kijeshiambao walihusika na mapinduzi, maslahi yao ya kibiashara sambamba na jamaa zao wa karibu". Rais Biden ameongeza kuwa wiki hii Marekani itabainisha awamu ya kwanza ya wale wataoguswa na vikwazo hivyo na vilevile inawazuia majenerali nchini Myanmar kuweza kuzifikia mali zenye thamani ya dola bilioni 1 katika fedha za serikali ya Myanmar zilizoko Marekani.

"Wakati maandamano yakiongezeka, unyanyasaji dhidi ya wale wanaodai haki zao za kidemokrasia haukubaliki na tutaendelea kuupinga. Watu wa Burma wanapaza sauti zao, na ulimwengu unaangalia. Tutakuwa tayari kuweka hatua za ziada na tutaendelea kushirikiana na washirika wetu wa kimataifa kuhimiza mataifa mengine yajiunge nasi katika juhudi hizi. "

Mapinduzi ya kijeshi ya Februari mosi ambayo yalimuondoa mamlakani kiongozi aliyechaguliwa kidemokrasia Aung San Suu Kyi, yalitokea chini ya wiki mbili baada ya Biden kuapishwa

Nchi za magharibi zimelaani mapinduzi hayo, lakini wachambuzi wanasema kwamba jeshi la Myanmar halitoweza kutengwa kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma, wakati kukiwa na uwezekano mkubwa wa China, India na mataifa jirani ya Kusini mwa Asia na Japan kutokata mahusiano na taifa hilo kutokana na umuhimu wake.

 

Credit:DW