Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bwana Gerald Kusaya  amewaeleza Wataalam kutoka Wizara ya Kilimo (Tanzania Bara) pamoja na wenzao wa na Wizara ya Kilimo Umwagiliaji Maliasili na Mifugo (Tanzania Visiwani) kuwa wanapaswa kujipongeza kuutekeleza na kuukamilisha Mradi wa Kuongeza Tija na Uzalishaji wa Mpunga (ERPP) kwa ufanisi mkubwa tangu aunze kutekelezwa Mwezi Aprili, 2015 hadi kukamilika kwake Mwezi Januari, 2021.

Mradi wa ERPP ulijikita katika kuongeza tija na uzalishaji wa zao la mpunga ambapo Mradi ulitekelezwa kwa ushirikiano wa Wizara hizo mbili za Tanzania Bara na Tanzania Visiwani.

Katibu Mkuu Kusaya akiwa sambamba na Katibu Mkuu mwenza wa Wizara ya Kilimo Umwagiliaji Maliasili na Mifugo Bi. Maryam Juma Abudulla ametoa pongezi hizo wakati akihitimisha kikao cha Wataalam kutoka Wizara hizo mbili waliokutana Jijini Dar es Salaam kwa siku mbili katika ukumbi wa Wizara ya Kilimo ili kujadiri masuala mbalimbali yenye lengo la kuongeza ushirikiano katika maeneo mbalimbali ya Sekta ya Kilimo.

Katibu Mkuu Kusaya amesema Wafadhiri wa Mradi huo wa ERPP Benki ya Dunia walitoa pongezi hizo hivi karibuni na kuongeza kuwa maeneo makuu yaliyokuwa yakitekeleza Mradi wa ERPP yatakuwa chachu ya kuongeza tija na uzalishaji katika zao la mpunga kwa Tanzania Bara na Tanzania Visiwani.

Katibu Mkuu Kusaya amewataka Wataalam kutoka pande hizo mbili za Wizara kujenga hoja katika kipindi hiki ili kuandaa maandiko yatakayosaidia Mradi huo kutekelezwa tena Tanzania Bara/Tanzani Visiwani katika mikoa na maeneo mengine ili kutoa wigo mpana kwa Watanzania kuendelea kunufaika na Mradi huo wa kuongeza tija na uzalishaji katika zao la mpunga.

“Benki ya Dunia wamefurahishwa kwa namna tulivyotekeleza Mradi wa ERPP na napenda kuwapongeza kwa namna mlivyosaidi katika kuhakikisha Mradi unakamilika kwa wakati na kwa kujibu wa vigezo vya Benki ya Dunia Mradi ulikamilika kwa asilimia 100.” Amekaririwa Katibu Mkuu.

Mradi wa ERPP ulianza kutekelezwa rasmi Mwezi Aprili, 2015 na uligharimu zaidi ya dola za Kimarekani milioni ishirini na mbili (Dola milioni 22) ambapo Tanzania Visiwani jumla ya skimu tatu zimejengwa na skimu sita zimekarabatiwa na kufanya eneo jipya la ujenzi wa skimu kufikia hekta 63 na hekta 132 ni skimu zilizokarabatiwa; Jumla ya Wakulima 4,922 wamenufaika na taknolojia ya kilimo shadidi (S.R.I).

Kwa upande wa Tanzania Bara. Halmashauri tatu za Wilaya za mkoa wa Morogoro zilizonufaika ni pamoja na Halmashauri ya wilaya ya Mvomero, Halmashauri ya wilaya ya Kilosa, Halmashauri ya Kilimbero Mji/Mlimba. Mradi wa ERPP umefanikisha katika ujenzi wa maghala mapya matano ya kuhifadhi chakula. Maghala hayo yanafanya jumla ya tani 6,700 zitakuwa zinahifadhiwa na Wakulima kabla ya kupelekwa sokoni.

Eneo lingine ni pamoja na ujenzi wa skimu tano katika Halmashauri hizo tatu za mkoa wa Morogoro ambapo skimu tano zilijengewa miundombinu na kufanya eneo lilijengwa katika maeneo ya skimu kufikia hekta 1,532.