Rais Dkt. John Magufuli ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuangalia namna ya kudhibiti biashara ya usafirishaji wa magogo kwenda nje ya nchi.

Akizindua shamba la miti la Silayo, Rais Magufuli amesema kumekuwa na udanganyifu kwenye biashara ya magogo na hivyo kuitaka wizara na TFS kusimamia eneo hilo ili serikali isipoteze mapato.

Amesema wengine wamekuwa wakisafirisha kwa njia za panya na hivyo kuikosesha serikali za mapato kutokana na biashara hiyo.

“Nakuomba waziri na Profesa [Silayo] mkasimamie eneo hili maana limekuwa na udanganyifu mwingi sana,” amesisitiza Rais.

Rais pia amewataka askari wa jeshi la uhifadhi kuendelea kulinda rasilimali hizo ili ziweze kuwa na manufaa kwa Taifa.