Sylvestre Ilunga Ilunkamba amejiuzulu rasmi kama waziri mkuu wa Jamuhuri ya kidemokrasi ya Congo, na kuwasilisha barua yake kwa Rais Félix Tshisekedi.

Bw Ilunga, ambaye ni mshirika mkuu wa mtangulizi wa Rais Tshisekedi, Joseph Kabila, ameongoza baraza la mawaziri la serikali ya Muungano kwa miezi 15.

Hata hivyo wabunge walipitisha kura ya kutokuwa na Imani na serikali yake Jumatano wiki hii na akapewa saa 24 awe amejiuzulu.

Kujiuzulu kwake kunatoa fursa kwa Rais Tshisekedi ya kuwateua washirika wake kama mawaziri.

Hadi sasa, utendaji wa Bw Tshisekedi umekuwa ukidhibitiwa na, muungano alionao na Bw Kabila ambao uliafikiwa wakati alipoingia madarakani miaka miwili iliyopita.

Ushindi wake katika uchaguzi mwezi Disemba 2018 ulisifiwa kama wa kihistoria-ambapo kulikuwa na makabidhiano ya kwanza ya utawala kwa njia ya amani ambayo hayakuwahi kushuhudiwa katika historia ya miongo sita nchini humo.