WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa ameipongeza Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) kwa kutoa ujuzi hususani kwa vijana ambao umewawezesha kujiajiri na kuajiriwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Ameyasema hayo jana (Jumatano, Januari 27, 2021) katika kikao chake na viongozi wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) na baadhi ya Mawaziri na Watendaji wa Serikali katika ukumbi wa Ofisi Ndogo ya Waziri Mkuu, Magogoni jijini Dar es Salaam.

Amesema sekta binafsi ndio injini ya maendeleo, hivyo Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano na taasisi hiyo kwa sababu inaitegemea sana katika kuhakikisha Taifa linasonga mbele kiuchumi.

Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kufanya maboresho ya sera, sheria na miongozo kwa ajili ya kuiwesha sekta hiyo kutekeleza majukumu yake kama ilivyokusudiwa kwa lengo la kuwa  na uchumi imara.

“Tuendelee kufanya kazi kwa bidii na tuzalishe bidhaa zenye ubora utakaotuwezesha kushindana kimataifa na kufikia uchumi wa juu. Pia naishukuru TPSF kwa kuzaisha ajira nyingi nchini.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama amesema Serikali imesikia hoja zote zilizotolewa na kwamba itazifanyiakazi na kutoa majibu kwa lengo la kuhakikisha sekta binafsi inatekeleza majukumu yake ipasavyo.

Naye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo amesema kwa sasa Serikali inaendelea kufanya mapitio ya sheria ya Uwekezaji na kwamba watarajie kuwa na sheria nzuri zaidi.

Awali, Mwenyekiti wa TPSF, Anjelina Ngalula alisema taasisi yao iko tayari kushirikiana na Serikali na kwamba itahakikisha kuwa inafanya Mapinduzi makubwa ya kibiashara nchini.

Mwenyekiti huyo ameiomba Serikali iandae sera maalumu kwa ajili ya maendeleo ya sekta binafsi itakayowezesha kushughulikia masuala yahusuyo sekta hiyo kwa urahisi.

Pia, alisema ushirikishwaji wa sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi mikubwa umekuwa ni wa kiwango cha chini, hivyo ameiomba Serikali iangalie upya suala hilo ili nao waweze kushiriki ipasavyo.