Na Atley Kuni, Mwanza
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Selemani Jafo ameoneshwa kufurahishwa na kupongeza Halmashauri ya Wilaya ya Misungi mkoani Mwanza kwa ubora wa ujenzi wa Hospitali ya Wilaya.

Mpaka sasa utekelezaji wa ujenzi huo wamekamilisha majengo ya maabara pamoja na jengo la wagonjwa wanje (OPD), baada yakupokea Sh milioni 500 katika awamu ya kwanza ya ujenzi huo.

Akizungumza baada ya kukagua ujenzi wa jengo hilo, Waziri Jafo, amesema: “ miongoni mwa halmashauri zinazo nishawishi kwenda kuomba fedha zingine kwa Mhe. Rais John Pombe Magufuli ni pamoja na Halmashauri hii ya Misungwi.

“Ndugu zangu mimi, niwapongeze kwa kazi kubwa mlio ifanya, haihitaji kuwa na darubini kubaini ubora wa majengo haya, ukiangalia milango, Vigae, vioo nk. mliyotumia lakini hata uimara wa maeneo mbalimbali hii inatia hamasa sana, pamoja na kwamba hamkuwepo katika bajeti iliyopita lakini mmeitendea haki fedha iliyoletwa, hongereni sana.”

Awali akitoa taarifa ya ujenzi huo, Mkurugenzi wa Halmashuri hiyo, Kisena Mabula, amesema kukamilika kwa hospitali hiyo, itakuwa na uwezo wa kuwahudumia watu wapatao 462, 855 wa wilaya hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyosomwa mbele ya Mhe. Waziri Jafo, inaonesha hadi kukamilika kwa Hospitali hiyo itatumia kiasi cha Sh 2, 076 468, 848, ambapo katika hatua za awali halmashauri ilipokea kiasi cha Sh milioni 500 kutoka Serikali kuu, zilizo tumika kukamilisha ujenzi wa jengo la maabara pamoja na jengo la wagonjwa wanje (OPD).

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. John Mongela, alimpongeza Mhe. Waziri Jafo kwa ziara yake katika Mkoa huo, huku akimhakikishia kuwa wataendelea kusimamia miradi yote kwa umakini mkubwa kadri watakavyokuwa wanaipokea.

“ Nikuhakikishie mheshimiwa waziri (Jafo) kuwa tutasimiamia kwa umakini miradi yote itakakayokuwa inatekelezwa katika mkoa wetu lakini pia tunatingatia maelekezo ya viongozi wote wa juu akiwepo Mhe. Rais mwenyewe.”

Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi ni moja kati ya Hospitali 97 zinazo endelea kujengwa nchi nzima

Awamu ya kwanza ya unejzu wa hospitali za wilaya ilijumuisha kujenga hospitali 67 na katika awamu ya pili inajumuisha ujenzi wa hospitali za wilaya 28 ambazo tayari ujenzi wake umanza ikiwa ni azima ya Serikali ya awamu ya tano kusogeza huduma karibu na wananchi.