Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt Damas Ndumbaro ameitangaza wilaya ya Chato mkoani Geita kuwa kitovu cha uhifadhi na utalii kwa Kanda ya Ziwa, kutokana na eneo hilo kuwa na vivutio vingi vya utalii, uhifadhi wa miti, hifadhi za Taifa pamoja na utalii wa ziwa.

Dkt Ndumbaro ameyasema hayo wakati akikagua shamba la miti la Biharamulo lililopo wilayani Chato mkoani Geita.

Kufuatia tangazo hilo, Waziri huyo wa Maliasili na Utalii amewataka Wafugaji na Wakazi wanaozunguka hifadhi za Taifa zilizopo wilayani humo kuacha mara moja kuingiza mifugo yao ndani ya hifadhi hizo.

Ameonya kuwa, mtu yeyote atakayeingiza mifugo ndani ya hifadhi hizo, akibainika mifugo yake itataifishwa.

Dkt Ndumbaro amewataka Wafanyakazi wa shamba hilo la miti la Biharamulo kuhakikisha wanalitunza ili liendelee kuwa la mfano kwa mashamba mengine.

Kwa upande wake Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Dos Santos Silayo amesema kuwa, Wakala huo utahakikisha ndani ya kipindi cha miaka ishirini ijayo wanamaliza kupanda miti katika shamba hilo ambalo ni la pili kwa ukubwa hapa nchini.