WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa Waziri Mkuu amesema Serikali inatarajia kutoa vitambulisho vipya vya Wamachinga vilivyofanyiwa maboresho ambavyo vitakuwa na picha ya muhusika na baadhi ya kumbukumbu binafsi zitakazomtambulisha na kumuwezesha kupewa huduma katika maeneo mbalimbali zikiwemo na taasisi za kifedha.

Amesema vitambulisho hivyo vitaanza kutolewa Aprili Mosi mwaka huu, hivyo amewataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya wahakikishe Wamachinga wanaendelea kufanya shughuli zao bila ya bugudha katika kipindi hiki ambacho muda wa matumizi ya vitambulisho vyao umekwisha.

Waziri Mkuu ameyasema hayo jana jioni (Alhamisi, Januari 28, 2021) wakati alipofunga Mkutano na Viongozi wa Wamachinga kutoka Mikoa yote Tanzania Bara, viongozi wa mabenki na baadhi ya Mawaziri na Watendaji wa Serikali katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.

Waziri Mkuu alisema vitambulisho hivyo vitakuwa na picha ya mhusika, hivyo haitawezekana kutumiwa na mtu mwingine na pia vitadumu kwa  miaka miwili hadi mitatu tofauti na vya sasa ambavyo vilikuwa vya mwaka mmoja.

“Serikali kupitia Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeamua kutoa vitambulisho rasmi ambayo vitawatambulisha popote na kupata huduma muhimu kama vile kutambulika na taasisi za fedha na maeneo muhimu.”

Kadhalika, Waziri Mkuu aliwaagiza viongozi wa Wamachinga wahakikishe wanakuwa na takwimu sahihi idadi ya Wamachinga ili iwe rahisi kuwahudumia. “Tuwe na kanzidata ya Wamachinga itarahisisha mawasiliano ndani ya Shirikisho la Wamachinga na Serikali.”

Waziri Mkuu alisema Wamachinga wajiunge pamoja kuanzia ngazi ya Vitongoji hadi Taifa ili waweze kuhudumiwa kwa urahisi. “Mkijiunga pamoja na kutambuliwa ni rahisi  kwa taasisi za kifedha kuwafikia na kuwapatia huduma za mikopo itakayowawezesha kukuza mitaji yenu.”  

Alisema Serikali imedhamiria kumhudumia na kumtumikia kila mwananchi wakiwemo Wamachinga kwa lengo la kuwawezesha kukuza biashara zao na kujikwamua kiuchumi, hivyo aliwataka wafanye kazi kwa bidii.

 (Mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU