Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Hussein Mwinyi amesisitiza kuwa Serikali yake itaendelea kuweka mazingira mazuri ya Uwekezaji ili kuwavutia Wawekezaji wengi wa ndani na nje ya Zanzibar.

Dkt Mwinyi ametoa kauli hiyo jijini Zanzibar wakati wa sherehe za maadhimisho ya miaka 57 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Amesema kuwa Uwekezaji ndio utakaoisaidia Zanzibar kuendelea kupiga hatua za kimaendeleo kwa haraka zaidi na kuifanya kuwa miongoni mwa maeneo bora Barani Afrika na hata Duniani.

Amesema lengo la Serikali yake ni kuhakikisha Zanzibar inarejea kuwa kitovu cha biashara katika eneo la Afrika Mashariki, hivyo Uwekezaji ndio utasaidia kufanikisha jambo hilo.

Dkt Mwinyi pia amewasisiriza Wakazi wote wa Zanzibar kuendelea kulipa kodi pamoja na Mamlaka husika kuendelea kubuni vyanzo vingine vya mapato , ambayo yatasaidia kuboresha huduma mbalimbali za kijamii.

Amesema baada ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12 mwaka 1964, Mapinduzi yanayosisitizwa sasa ni yale ya sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja na elimu na afya ambayo yana mchango mkubwa katika maendeleo ya Zanzibar.

Dkt Mwinyi pia amekemea vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinavyoendelea kushamiri na kuitia doa Zanzibar na kutaka wale wote wanaobainika kutenda vitendo hivyo wachukuliwe hatua za kisheria.