Nay Akiuka Kiapo cha Mama Yake ya Kutoa Video za Kimafreemanson


STAA mtata wa Hip Hop Bongo, Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’ amekiuka kiapo alichomuahidi mama yake. Nay ameachia ngoma mpya inayokwenda kwa jina la Go Baba ambayo baadhi ya vipande katika video hiyo inaonesha matendo ya kutisha kama vile Nay kunywa kimiminika kinachofanana na damu.

Mwaka jana, Nay aliachia wimbo wake unaoitwa Mungu Yuko Wapi ambao uliibua utata wa kimapokeo ikiwemo ya kupingwa na baadhi ya mashabiki kwa kile kilichotajwa kuwa mashairi yake yalikuwa yakikosoa uwepo wa Mungu.

Moto zaidi kuhusu wimbo huo ulipamba baada ya Nay kuachia video yake ambayo kwa kiasi kikubwa ilikuwa imetawaliwa na picha zenye mahadhi ya kutisha (horror) mfano picha zinazoonesha watu wananyongwa na hata uhariri wa rangi wa video hiyo ulifanywa kwa namna ya ambayo filamu nyingi za kutisha hufanya.

Video hiyo ilileta utata siyo tu kwa mashabiki wake, bali hadi kwa mama yake, Nay. Mama huyo aliibuka na kudai kuwa video hiyo ilimchukiza na kumtaka Nay aifute haraka.

Hata hivyo, Nay hakuifuta licha ya kwamba alikiri kupewa maeleko hayo na mama yake ambapo alimuapia kwamba hatafanya tena video au wimbo wa aina hiyo.

“Ni kweli bimkubwa aliniambia niifute video ya Mungu Yuko Wapi, lakini hajanipa sababu, alisema tu niifute,” alisema Nay wakati huo.

Lakini Januari 7, mwaka huu, Nay amerudia jambo kama hilo baada ya kuachia video ya wimbo wake huo ambayo inafanana kwa kiasi kikubwa na video ya Mungu Yuko Wapi.

Baadhi ya vipande katika video hiyo mpya iliyoongozwa na muongozaji Joowzey kutoka Tanzania inaonesha matendo ya kutisha kama vile Nay kunywa kimiminika kinachofanana na damu, baadhi ya madansa katika video hiyo kupaka rangi za kutisha usoni, uvaaji wa mashuka mekundu na meupe kama kwenye filamu za kutisha, lakini pia hata uhariri wa rangi umefanyika kwa aina ileile iliyofanyika kwenye video ya Mungu Yuko Wapi.

Video hiyo inakaribia kuwa na watazamaji zaidi ya laki 2 ndani ya muda mfupi kwenye Mtandao wa YouTube.

STORI; KHADIJA BAKARI, DAR