Mahakama nchini Uganda imeamuru vikosi vya usalama kuacha kuizingira nyumba ya kiongozi wa upinzani Bobi Wine, ambaye kifungo chake cha nyumbani tangu uchaguzi wa rais uliofanyika katikati ya mwezi huu kimesababisha shinikizo la kimataifa. 

Wakili wa Wine, George Musisi amesema jaji ameamuru kuwa serikali na mashirika yake ya usalama yaondoke mara moja kwenye makazi ya kiongozi huyo na haki yake ya kuwa huru irejeshwe haraka. 

Musisi amesema jaji pia ameamuru kuwa kama kuna tuhuma zozote muhimu dhidi ya Wine, anapaswa kufikishwa mahakamani au kituo cha polisi. 

Msemaji wa polisi Patrick Onyango amesema hawezi kuzungumzia hilo kwa sababu uamuzi huo wa mahakama haujamfikia. 

Wanajeshi walimzuia mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 38 aliyegeuka kuwa mwanasiasa, kuondoka nyumbani kwake mjini Kampala, tangu alipopiga kura katika uchaguzi wa Januari 14 

 

Credit: DW