Waziri wa kilimo.Prof.Adolf Mkenda amefanya mkutano na waandishi wa habari kuhusiana na hali ya uzalishaji wa sukari hapa nchini.

Prof.Mkenda amesema kuwa  uzalishaji  wa sukari hapa nchini umekuwa ukiongezeka katika kipindi cha miaka mitano uzalishaji wa sukari umeongezeka kwa asilimia 78.3 (kutoka tani 295,775 mwaka 2015/2016 hadi tani 377,527 zinatarajia kuzalishwa msimu wa 2020/2021)

Hata hivyo Prof.Mkenda amesema kuwa mafanikio haya ya kuongezeka kwa uzalishaji ni matokeo ya utekelezaji wa sera na mikakati ambayo serikali imeweka kuhakikisha wazalishaji wana mazingira mazuri ya kufanya upanuzi wa mashamba na wakulima kuongeza tija.

Aidha ,katika msimu wa mwaka 2020/2021 jumla ya tani 377,527 za sukari zitazalishwa kutoka kwenye viwanda vilivyopo vya Kilombero  Sugar Company Ltd,Mtibwa Sugar Estate, Kagera Sugar Ltd, TPC Ltd na Manyara Sugar Ltd. Pia  amesema kuwa mahitaji ya sukari kwa ujumla hapa nchini kwa matumizi ya kawaida na viwandani ni tani 655,000 kwa mwaka.

Pof.Mkenda ameendelea kusema kuwa ili kuongeza uzalishaji Serikali imejipanga kuboresha miundombinu ya umwagiliaji kwa wakulima wadogo, viwanda viongeze uwezo wa kuchakata miwa inayozalishwa na kuongeza tija  kwa uwepo wa mbegu bora na viuatilifu.

Kutokana na uhaba wa sukari uliopo na miwa ya wakulima kubaki mashambani bila kuvunwa kwa sababu ya ufanisi na uwezo mdogp wa viwanda, serikali imeelekeza Kiwanda cha Kilombero na viwanda vingine kuongeza na kuimarisha uwezo wa uchakataji wa miwa ili kunusuru hasara kubwa wanayoipata wakulima kwa kutovuniwa miwa yao na kupelekwa kuchakatwa viwandani.Alisema Prof. Mkenda

Serikali haitosita kuchukua hatua ya kuruhusu mwekezaji mwingine kujenga kiwanda cha kati kimoja au viwanda vidogo viwili endapo mwekezaji aliyopo sasa katika bonde la Kilombero atashindwa kufanya upanuzi unaostahili kwa wakati ili miwa ya wakulima wadogo takribani tani 200,000 inayobaki katika bonde la kilombero ipate soko la uhakika.