Mabaraza ya bunge la Marekani yamemthibitisha rais mteule Joe Biden kuwa mshindi wa rais katika uchaguzi uliofanyika Novemba.

Mabaraza hayo mawili yalitupilia mbali matakwa ya wapambe wa Trump kwamba matokeo katika majimbo ya Arizona na Pennsylvania yabatilishwe. 

Baada ya kukamilika kwa mchakato huo, seneta Amy Klobuchar alisema wameweka rekodi kwamba Biden atakuwa rais na Harris makamu wake kulingana na kura ambazo wamepewa.

Punde baada ya ushindi wa Biden kuidhinishwa, Rais Trump ametoa taarifa akiahidi makabidhiano ya amani ya madaraka huku akidokeza kuwa atasalia kwenye siasa, hatua inayoibua gumzo kwamba atataka kuwania tena urais mwaka 2024.