Na: Mwandishi Wetu – Dodoma
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amesema Ofisi ya Waziri Mkuu imejipanga kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kasi zaidi ili kuendana na kasi ya serikali ya Awamu ya Tano.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wenye dhamana ya Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama mara baada ya kupokelewa rasmi katika Ofisi ya Waziri Mkuu iliyopo Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma hii leo Disemba 10, 2020.

Waziri Mhagama alieleza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu imejipanga kuhakikisha inatekeleza majukumu na kazi zake kwa kasi zaidi ili kutimiza malengo ambayo wananchi wanayatarajia ikiwemo kutoa huduma bora na kutatua changamoto mbalimbali za wananchi, hivyo aliwataka watumishi wa Ofisi hiyo kufanya kazi kwa uzalendo na bidii.

“Tunakila sababu ya kujipanga sawasawa ili kuhakikisha yale tuliyofanikiwa tunayalinda na maeneo yale ambayo hatujafanya vizuri tunayafanyia kazi kwa kuboresha utendaji zaidi,” alisisitiza Waziri Mhagama

Aidha, alieleza kuwa ujio wa Naibu Mawaziri wapya katika Ofisi hiyo ni ishara tosha kuwa sasa watumishi inabidi wawe katika hari mpya na nguvu mpya ili waendelee kutekeleza majukumu yao kwa ufasaha na kutimiza malengo waliyokusudia.

Sambamba na hayo, Waziri Mhagama aliwahiza watumishi wa Ofisi hiyo kushirikiana pamoja na viongozi na kwa pamoja wajenge tabia ya kukumbushana uwajibikaji wa viwango wa hali ya juu na kutambua miiko ya utekelezaji wa majukumu yao kwa mujibu wa sheria za utumishi wa Umma.

Kwa upande wake, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Ajira) Mhe. Patrobas Katambi amesema kuwa katika muhula huu wa pili anaimani kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaenda kutekeleza majukumu yake vizuri huku akiongezea kuwa ofisi hiyo itaendelea kushirikiana na Wizara nyingine mbalimbali katika kufanikisha gurudumu la maendeleo ya Taifa.

Naye, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Wenye Ulemavu) Mhe. Ummy Nderiananga amesema kuwa atahakikisha watumishi wa ofisi hiyo kwa pamoja wanashirikiana katika kushughulikia masuala mbalimbali ikiwemo yanayohusu wenye ulemavu ili kufanikisha malengo waliyokusudia kwa pamoja.