Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita, imewahukumu kunyongwa hadi kufa, washtakiwa 4, akiwemo Alphan Kyalubota, Epafla Mapinda, Mashimu Omary na Kululinda Richard, kwa kosa la kumuuwa kwa kukusudia aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA, mkoani humo Alphonce Mawazo, aliyeuawa mwaka 2015.


Hukumu hiyo imetolewa  Desemba 24, 2020, na Hakimu Mkazi Mwandamizi mwenye mamlaka ya ziada Frank Mahimbari, baada ya kujiridhisha kutokana na ushahidi uliotolewa mahakamani hapo kutoka kwa mashahidi upande wa Jamhuri.

Katika shauri hilo namba 9 la mwaka 2019, mshatakiwa wa nne, Habibu Feruzi, ameachiwa huru baada ya ushahidi uliotolewa mahakamani hapo kushindwa kuthibitisha kuhusika kwake kwenye mauaji hayo ya kukusudia hivyo kutokuwa na kesi ya kujibu.

Baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa waliojitokeza kufuatilia kesi hiyo, wamesema kuwa wameridhishwa na hukumu hiyo huku wakiipongeza serikali kwa kutenda haki kwa watu wote bila kuangalia itikadi ya chama.