Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mwita Waitara amewataka wachimbaji wadogo kuwa na sehemu ya pamoja na kuchenjua dhahabu ili kudhibiti kusambaa kwa mabaki ya zebaki.

Waitara alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza kwenye mkutano wa hadhara na wachimbaji wadogo kwenye mgodi mdogo wa Blue Leaf uliopo mkoani Geita alipofanya ziara ya kikazi.

Naibu waziri huyo alisema wachimbaji wanapaswa kuwa na sehemu moja kwa shughuli za uchenjuaji hatua itakayosaidia kudhibiti maji yasisambae kwenye mazingira hivyo kuathiri binadamu, wanyama na mimea.

“Lengo la Serikali sio kuwakwamisha wachimbaji wadogo lakini pia wanapaswa kutekeleza kanuni na taratibu hivyo wana nafasi ya kuhakikisha wanatunza mazingira kwa kupanda miti maeneo wanayokatwa kwa kuwa wanatumia sehemu kubwa ya miti katika shughuli zao,” alilisitiza.

Pamoja na mambo mengine katika ziara hiyo Waitara alipanda mti kuhamasisha wachimbaji wengine wafanye hivyo kwa kuwa wanatumia sehemu kubwa kuikata. Pia alimpongeza mwenyekiti wa mgodi huo, Christopher Kadio kwa kuzingatia kanuni za mazingira zikiwemo kupanda miti katika maeneo hayo.

Aidha, akizungumza katika kikao na maafisa mazingira kutoka halmashauri za Mkoa wa Geita alizitaka halmashauri hizo kujenga madampo ya kisasa kwa ajili ya taka ngumu ili kutunza mazingira.

Waitara alisema pia zinapaswa kuweka mfumo unaoeleweka wa maji taka na taka ngumu ili wananchi wajue taka hizo zinatupwa wapi na kushirikiana na wanaozalisha taka hizo hususan za plastiki kuzilejeza.a agizo hilo jana

Naibu Waziri Waitara amefanya ziara mkoani Geita kwa lengo la kuelimisha umma kuhusu juhudi za Serikali katika kulinda hifadhi ya mazingira, kuhamasiaha usafi wa mazingira, upandaji miti pamoja na kukagua uzingatiaji wa Sheria ya Hifadhi ya Mazingira ya mwaka 2004.