MWANAMUZIKI wa Tanzania, Vanessa Mdee, amevalishwa pete ya uchumba na mpenzi wake Rotimi ambaye ni msanii wa filamu ambapo wote kwa sasa wanaishi nchini Marekani.

‘Videos clips’ ambazo zimepostiwa kwenye mitandao ya kijamii zimeonyesha Rotimi akiwa amepiga magoti mbele ya Vanessa huku akimvalisha pete hiyo ya uchumba, kisha wakakumbatiana na kuanza kupigana mabusu.
 
Vanessa amethibitisha hilo kupitia ukurasa wake wa Instagram ambapo ameweka video mbili moja ikionesha pete aliyovishwa huku nyingine ikiwa ni kipande cha video ya mahojiano aliyowahi kufanya na moja ya vyombo vya habari na kusema ilimgharimu siku mbili tu kujua kwamba Rotimi ndiye atakayekuja kuwa mume wake.

“Mwaka mmoja na nusu uliopita dunia ilicheka niliposema kuwa nilijua kuwa wewe utakuja kuwa mume wangu muda mfupi baada ya kukufahamu, sikuwalaumu kwani hisia unayoipata pale unapokutana na mpenzi wa maisha yako si ya kawaida na haiwezi kuelezeka lakini pia wao walikuwa wakimfahamu Vanessa ambaye hakuwa na mpango wa kuolewa kwa wakati huo,” ameandika Vanessa.

Rotimi naye kupitia ukurasa wake wa Instagrama ameweka video fupi ya pete aliyomvalisha Vanessa akiambatanisha na ujumbe unaoelezea namna anavyompenda mrembo huyo.

“Unanifanya niwe mwanaume bora. Nina deni kwa Mungu kwa kunipa wewe na nitamlipa kwa kukupenda na kukupa kila kitu unachostahili, nakupenda,” ameandika Rotimi.

Uhusiano wa wawili hao ulianza mwaka 2019 baada ya Vanessa kuachana na aliyekuwa mpenzi wake, mwanamuziki wa Tanzania, Jux.

Kwa sasa Vanessa ambaye mwezi Juni alitangaza kuachana na shughuli za muziki anaishi Marekani pamoja na mwanume huyo na mara kadhaa amekaririwa akimsifia kuwa ni mwanaume aliyefanya aitambue thamani ya maisha yake.

Mwanzoni mwa mwezi wa kumi mwaka 2020, Vanessa  na Rotimi walishea picha mitandaoni zikiwaonyesha wamechorana ‘tattoo’ zenye majina yao kwenye miili yao.