Jamuhuri ya Afrika ya Kati imetangaza Jumatatu (Desemba 21) kuwa Rwanda na Urusi zimetuma wanajeshi wao baada ya shambulio la makundi ya waasi lililodaiwa na na serikali kama "jaribio la mapinduzi"kabla ya Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Jumapili.

Katika nchi hii isiyo na utulivu, inayokumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vimesababisha maafa makubwa, makundi yenye silaha yanadhibiti zaidi ya theluthi mbili ya nchi hiyo.

Makundi matatu kati ya makundi yenye nguvu zaidi nchini Jamhuri ya afrika ya Kati yalishambulia, siku ya Ijumaa, barabara muhimu zinazoelekea mji mkuu, Bangui, na kutangaza muungano wao.

Siku ya Jumamosi serikali ya Bangui ilimshtumu rais wa zamani François Bozizé kwa "kujaribu kupindua serikali" kwa "nia dhahiri ya kuandamana na vikosi vyake katika mji wa Bangui" wakati uchaguzi wa Jumapili unaandaliwa kote nchini.

Hata hivyo rais anayemaliza muda wake, Faustin Archange Touadéra anapewa nafasi kubwa ya kushinda, baada ya François Bozizé kukataliwa kugombea kutokana na kuwa hatimizi vigezo vya kuwania katika uchaguzi huo.

Kwa kuunga mkono serikali, "Urusi imetuma mamia ya wanajeshi kutoka vikosi vya kawaida, na vifaa vikubwa" kama sehemu ya mkataba wa ushirikiano wa pande mbili, msemaji wa serikali Angel Maxime Kazagui ameambia shirika la habari la AFP.