Kufuatia taarifa zinazo sambaa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu askari wa  mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania TAWA kumuua Simba katika kijiji cha Ngwala wilayani Songwe ili kunusuru maisha ya watu na kuonekana kuwa wamekiuka haki za wanyama na kuleta mjadala katika mitandao ya kijamii mamlaka hiyo imetoa ufafanuzi kwamba ilikuwa inatekeleza majukumu yake.
 
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari afisa wanyamapori mwandamizi udhibiti wa wanyamapori wakali na waharibifu TAWA Wilbright Munuo, amesema mamlaka inakemea vikali taarifa za opotoshaji zinazo sambaa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu udhibiti wa wanyamapori wakali na waharibifu.


Amesema jamii inatakiwa kufahamu kuwa kazi zinazofanywa na wataalam wa TAWA zinafanywa kwa kuzingatia sheria ya uhufadhi ya wanyamapori namba 5 ya mwaka 2009, hivyo hazipaswi kubezwa kwani kufanya hivyo ni kuingilia majukumu ya mamlaka.
 
Aidha amesema sheria ya uhifadhi wanyamapori namba 5 ya mwaka 2009 inatambua umuhimu wa kulinda maisha ya watu na mali zao dhidi ya wanyamapori wakali na waharibifu, licha ya mamlaka kutumia mbinu  mbalimbali za kuthibiti wanyamapori hao katika vijiji ikiwemo kutishia kwa risasi.


Pia amesema njia nyingine zinazotumika ni kuwapeleka wanyama wakali na waharibifu katika bustani na ranchi za wanayapori kwa kuzingatia mahitaji Ili kuepusha taharuki kwa wananchi.
 
Amesema mamlaka katika kuhimarisha usalama wa maisha ya watu na mali zao imekuwa ikihamisha wanyamapori waliokuwa wakivamia maeneo ya wananchi na kuwarudisha katika maeneo ya hifadhi.

‘‘Mwezi mei,2017 Tembo wanne walivamii maeneo ya chuo kikuu cha dodoma waliwarudisha hifadhini bila ya kuleta madhara kwa wananchi,pia mwezi February 2020 TAWA kwa kushirikiana na taasisi ya utafiti wa wanyamapori Tanzania TAWILI tuliwahamisha Simba 36 ambao waliua ng`ombe zaidi ya 100 katika Vijiji cha Kwitete,makundusi,iharara,robanda,pakinyigoti,nichoka na maeneo ya hifadhi ’’Alisema Wilbright Munuo.
 
Vilevile Munuo ameongeza kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja wa  2020 pekee jumla ya matukio 993 ya wanyamapori kuvamia maeneo ya wananchi yaliripotiwa katika vituo vya TAWA ambapo wanyamapori hao walirudishwa kwenye maeneo ya hifadhi.