Mgombea urais wa Uganda Robert Kyagulanyi, maarufu kama Bobi Wine, amesema kuwa anaanza tena kampeni zake Alhamisi, baada ya kukutana na Tume ya uchaguzi.

“Leo tunaanza tena kampeni zetu Kibuku, Budaka na Manafwa! Lengo letu ni kupata uhuru,” Bobi Wine amesema.


Aliongeza: “Hata nikitembea katika mabonde ya kivulivuli cha kifo, Sitaogopa ubaya wowote, kwasababu Mungu yuko nami!”


Tofauti na mavazi yake aliyokuwa akivalia kila siku leo amevalia koti na kofia ya kuzuia risasi yaani Bullet Proof.


Bobi Wine ameviambia vyombo vya habari kuwa aliitaka Tume ya Uchaguzi kulinda wanasiasa wa upinzani dhidi ya vikosi vya usalama au ijiuzulu.


Aliongeza kuwa pia alitaka tume ya uchaguzi kisitisha vikosi vya usalama kufunga barabara na maeneo ya kufanya uchaguzi ambako kunazuia upinzani kuzungumza na wapiga kura.


Idadi kubwa ya maafisa wa polisi walikuwa wamezunguka majengo ya tume baada ya kupata taarifa kuwa Bobi Wine anatarajia kutembelea jengo hilo.


Bobi Wine alisitisha kampeni zake Jumanne baada ya timu ya kampeni yake kujeruhiwa na gari lake kuvamiwa, huku vikosi vya usalama vikitawanya wafuasi wake mashariki mwa Kampala.


Afisa wa polisi ambaye hutolewa na tume ya uchaguzi kwa kila mgombea urais pia naye alijeruhiwa.


Imesalia takriban mwezi mmoja kufika kwa uchaguzi mkuu unaofanyika Januari 2021, na wapinzani nchini Uganda pamoja na wafuasi wao wamekuwa wakizuiliwa kufanya mikutano ya hadhara kwasababu vikosi vya usalama vinajitahidi kuhakikisha maagizo ya wizara ya afya juu ya kukabiliana na virusi vya corona yanafuatwa.