Kesi inayomkabili mchekeshaji maarufu nchini Tanzania, Idriss Sultan na wenzake wawili ya kuchapisha maudhui mtandaoni bila kuwa na kibali kutoka TCRA, imeshindwa kuendelea baada ya shahidi upande wa Jamhuri kutokufika Mahakamani hapo.


Mbali nan Idris Sultan, washtakiwa wengine ni mfanyabiashara Doctor Ulimwengu (28) mkazi wa Mbezi Beach na Isihaka Mwinyimvua (22) ambaye ni msanii na mkazi wa Gongolamboto.



Akieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Wakili wa Serikali Neema Mushi, amedai kuwa shahidi aliyetakiwa kuwepo hajafika hivyo anaomba tarehe nyingine na watatoa "summonce" ili tarehe nyingine aweze kufika Mahakamani, ambapo kesi hiyo itasikilizwa tena Januari 26,2021.



Hata hivyo upande wa utetezi uliowakilishwa na Wakili Jebra Kambole na Maria Mushi haukuwa na pingamizi lolote.



Kwa mujibu wa hati ya mashtaka,washtakiwa wanadaiwa kutenda kosa hilo kati ya Machi 8, 2016 na Machi 13, 2020 katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam.



Inadaiwa siku hiyo ya tukio, kwa kutumia 'Online Tv" inayojulikana kwa jina la Loko Motion, walichapisha maudhui katika mtandao huo bila ya kuwa na kibali kutoka TCRA, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.