Rais wa Zanzibar,  Dk Hussein Mwinyi amemteua mwenyekiti wa Chama cha ACT- Wazalendo,  Maalim Seif Sharif Hamad kuwa makamu  wa kwanza wa Rais Zanzibar.

 Uteuzi huo umeanza jana Jumapili Desemba 6,  2020 na kutangazwa na katibu mkuu kiongozi wa Zanzibar,  Dk Abdulhamid Yahya Mzee.

"Kwa kuzingatia matakwa ya kifungu cha 9(3) cha katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kinachosomeka kwamba,   muundo wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar utakuwa wa Umoja wa Kitaifa na utendaji wa kazi zake utafanywa katika utaratibu utakaohakikisha kuendelezwa kwa umoja nchini na lengo la kufikia demokrasia."

"Rais wa Zanzibar amemteua Maalim Seif kuwa makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar, " inaeleza taarifa hiyo.

Uteuzi huo umekuja saa chache baada ya kumalizika kwa kikao cha kamati kuu ya ACT-Wazalendo kilichoridhia kushiriki katika uundwaji wa Serikali hiyo.