Mkazi wa Mbagala Kizuiani, Faraji Omary(26) amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kujibu mashtaka manne, likiwemo la kusambaza picha za ngono na kusambaza machapisho yenye ujumbe mchafu unaoharibu maadili ya jamii.

Mshtakiwa huyo amefikishwa mahakamani hapo, jana Desemba 29, 2002 na kusomewa mashtaka yake na wakili wa Serikali Adolf Ulaya, mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Rashid Chaungu.

Wakili Ulaya amedai kuwa mshtakiwa anakabiliwa na kesi ya jinai namba 173/2020 na kwamba ameunganishwa na mshtakiwa mwenzake aitwaye Aisha Kiula, ambaye alisomewa mashtaka kama hayo, Desemba 23, 2020.

Akimsomea mashtaka yake, wakili Ulaya amedai kuwa mshtakiwa anadaiwa kutenda makosa yake kati ya Desemba 4 na Desemba 14, 2020 katika eneo la Kariakoo Jiji hapa.

Hata hivyo, mshtakiwa amekana mashtaka yake na kesi yake imeahirishwa hadi Januari 11, 2021 itakapotajwa.

Mshtakiwa amerudishwa rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana.