KING wa Bongo wa Fleva, Ali Saleh Kiba ‘King Kiba’ ana kishindo kingine ambacho ni balaa la kufunga mwaka huu wa 2020 unaweza ukaita kubwa na nusu.

 

Taarifa ikufikie kuwa, baada ya ngoma yake ya Mediocre iliyotikisa vilivyo, kabla ya mwaka huu kugeuka, basi kuna bonge la kolabo ya wimbo mwingine mkali unaokwenda kwa jina la Nakupenda.

 

Wimbo huo amefanya na DJ maarufu wa nchini Afrika Kusini aitwaye DJ SBU ambaye ni maarufu mno nchini Afrika humo. Wimbo huo upo ndani ya albam ya DJ SBU ambao utaanza kusikika muda wowote ndani ya mwezi huu,ambapo albam hiyo itakuwa inaachiwa rasmi.

 

Kwa mujibu wa DJ SBU amefurahi kufanya wimbo huo ambao ni namba tisa kwenye albam yake hiyo. Baadhi ya vipande vifupi vya utengenezaji wa video ya wimbo huo, Kiba anasikika akiimba kwa lugha ya Kingereza na ndiyo itakuwa kolabo yake kubwa kwa mwaka huu na kwamba itakwenda kufungua milango zaidi ya Bongo Fleva.

 

Mmoja wa watu wa Lebo ya Kings Music inayomilikiwa na Kiba alilithibitishia Gazeti la IJUMAA WIKIENDA kuwa, ngoma hiyo inakwenda kujibu ile iliyofanywa na hasimu wake kimuziki, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ na mtu mzima kutoka Kongo, Koffi Olomide inayokwenda kwa jina la Waah.