Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limefanikiwa kukamata gari lenye namba za usajili namba T.634 CAS aina ya Corola likiwa na vipodozi vya aina mbalimbali vilivyopigwa marufuku vyenye viambata sumu.

Ni kwamba mnamo tarehe 28/11/2020 majira ya saa 04:00 usiku, kikosi maalum cha kuzuia na kupambana na uhalifu kikiwa doria barabara kuu ya Mbeya – Tunduma walilisimamisha gari namba T.634 CAS aina ya Corola lakini dereva wake aligoma kusimama. Katika mfuatiliaji dereva huyo alikimbia na kulitelekeza gari.

Katika upekuzi uliofanyika ndani ya gari hilo zilikutwa katoni 34 ya vipodozi aina mbalimbali vilivyopigwa marufuku nchini zenye viambata sumu.

Upelelezi unaendele kubaini mmiliki wa gari hilo pamoja na mwenye bidhaa hizo zilizopigwa marufuku nchini kwa hatua zaidi za kisheria.

KUKAMATWA WATUHUMIWA WA WIZI KWA NJIA YA MTANDAO.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa saba [07] kwa tuhuma za wizi na utapeli kwa njia ya mtandao ambao ni:-

  1.     MASOUD PIUS [23] Mkazi wa Mwanyanje.
  2.     GIFT JOSEPH [22] Mkazi wa Igawilo.
  3.     NOEL MBUNDA [24] Mkazi wa Igawilo.
  4.     HANCE WILLIAM [24] Mkazi wa Isyesye.
  5.     ENOCK MAHENGE [22] Mkazi wa Iganjo.
  6.     JACKSON EMMANUEL [23] Mkazi wa Nsalaga.
  7.     BAHATI STEVEN [22] Mkazi wa Nsalaga.

Watuhumiwa walikamatwa mnamo tarehe 07.12.2020 majira ya saa 00:30 usiku huko Isyesye na Uyole Jijini Mbeya na baada ya kupekuliwa walikutwa na laini 49 za mitandao ya Airtel, Vodacom, Tigo, TTCL na Halotel ambazo wamekiri kuzitumia kutapeli na kuibia watu. Upelelezi wa shauri hili unaendelea na mara baada ya kukamilika watafikishwa mahakamani.

Imetolewa na:
 [ULRICH MATEI-SACP]
KAMANDA WA POLISI MKOA WA MBEYA