Na Amiri Kilagalila,Njombe
Jeshi la polisi mkoa wa Njombe linamshikilia mfanyabiashara wa vyuma chakavu eneo la mizani mjini Makambako aliefahamika kwa majina ya Anania Msemwa baada ya kukutwa na vyuma vya reli ya Tazara na vingine vinavyodaiwa kuibwa kwenye mradi wa ujenzi wa barabara ya Moronga-Makete

Kamanda Issa amebainisha baadhi ya miundombinu iliyokamatwa kuwa ni pamoja na vyuma vya reli ya Tazara pamoja na vyuma ambavyo vimeibwa katika miradi ya ujenzi wa barabara ya Moronga -Makete ndani mkoa wa Njombe.

“Kilichopatikana hapa Makambako ni vyuma vya Reli ya Tazara kwa hiyo amekamatwa mtu ambaye alikuwa ameviweka nyumbani kwake na huyu mtu ana kibali cha kufanya biashara ya kununua vyuma chakavu na vyuma hivi vimeshatambuliwa vinatokana na reli na reli inayopatikana hapa ni ya Tazara”alisema kamanda Issa

Pamoja  na hayo Jeshi la polisi linamshikilia Anania Msemwa mwenye umri wa miaka 50 mfanyabiashara na mkazi wa Njombe ambaye anajihusisha na ununuzi wa vyuma chakavu baada ya kukutwa na vyuma hivyo.

“Na tumeweza kukamata vyuma vingine 17 vizito kweli kweli aliyekamtwa navyo anaitwa Anania Msemwa.huyu ni mfanyabiashara ananua vvyuma chakavu eneo la mizani Makambako,na vyuma hivi vimetoka kwenye Krushia ya kupasua kokoto kwenye mradi wa kutengeneza barabara inayotoka Moronga-Makete”aliongeza kamanda Issa

Kamanda Issa amewataka wakazi wa Njombe kuheshimu miradi ya serikali inayotekelezwa katika mkoa huo kwa kutoa taarifa na kuwafichua watu wote wanaojihusisha na kuhujumu miradi hiyo kwa kuiba mafuta , saruji na baadhi ya vifaa vinavyotumika katika ujenzi wa miradi hiyo.