CHAMA cha ACT – Wazalendo, kimekubali kuungana na Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), visiwani Zanzibar. 


Pia, kimeazimia kuwaruhusu Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, Wabunge na Madiwani wa chama hicho waliochaguliwa kwenda kukiwakilisha chama na wananchi waliowachagua.

Akizungumza na waadishi wa habari leo tarehe 6 Desemba 2020, jijini Dar es Salaam, Ado Shaibu ambaye ni Katibu Mkuu wa chama hicho, amesema uamuzi huo uliofanywa na Kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho kilichoketi tarehe 5 Septemba 2020, umezingatia maoni ya baadhi ya wananchi, wanachama na viongozi wa chama hicho.

Akisoma maazimio hayo, Ado amesema; “Mosi kamati kuu ya chama chetu imeazimia wawakilishi wachache kwa maana ya madiwani, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Wabunge ambao wametangazwa kushinda waruhusiwe kushiriki kwenye vyombo vyao vya uwakilishi,” amesema Ado na kuongeza

“Pili Kamati Kuu ya chama chetu imeridhia chama kushiriki katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar na imeielekeza Kamati ya Uongozi ya chama chetu kupendekeza jina la mwanachama atakayekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar,” amesema Ado akisoma maazimio ya kamati kuu ya chama hicho.